CPA MURO: TUFANYE KAZI KWA UMOJA NA USHIRIKIANO ILI KUIMARISHA UTENDAJI WA COASCO
CPA MURO: TUFANYE KAZI KWA UMOJA NA USHIRIKIANO ILI KUIMARISHA UTENDAJI WA COASCO
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO), CPA Alphonce Muro, ameihimiza Menejimenti ya Shirika kufanya kazi kwa umoja, mshikamano, ushirikiano na uwajibikaji ili kuimarisha utendaji wa Shirika na kufikia matarajio ya wadau.
CPA Muro ameyasema hayo leo, Septemba 3, 2026, katika kikao chake cha kwanza na Menejimenti ya COASCO tangu kuteuliwa na Bodi ya Wakurugenzi kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika. Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya COASCO jijini Dodoma.
“COASCO haiwezi kutegemea mtu mmoja, hivyo tufanye kazi kwa bidii, umoja, mshikamano na ushirikiano ili kufikia matarajio makubwa ya wadau ya kuona sekta ya ushirika ikiendelea kukua,” amesema CPA Muro.
Aidha, CPA Muro amesisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa viwango vya ubora wa kimataifa, kuhakikisha ukaguzi unaleta matokeo yenye manufaa kwa wadau, kuimarisha matumizi ya teknolojia, kuendeleza utamaduni wa Shirika, kujenga mahusiano mazuri na wadau pamoja na kuimarisha taswira ya COASCO.
